Baruku 5

1 Ee Yerusalemu, vua vazi lako la huzuni na mateso,

ukavae milele uzuri wa utukufu wa Mungu.

2 Jivike joho la uadilifu utokao kwa Mungu;

vaa kichwani taji la utukufu wa Mungu wa milele.

3 Maana Mungu atadhihirisha fahari yako kila mahali duniani.

4 Mungu atakupa jina hili milele:

“Amani kwa uadilifu; fahari kwa uchaji wa Mungu.”

5 Inuka, ee Yerusalemu, usimame milimani,

tazama upande wa mashariki,

uwaone watoto wako wamekusanywa kutoka mashariki na magharibi,

kwa amri ya Mungu Mtakatifu.

Wanashangilia kwani Mungu amewakumbuka.

6 Waliondoka kwako kwa miguu,

wakichukuliwa na maadui zako.

Lakini Mungu atawarejesha tena kwako

wakiwa wamebebwa kwa fahari kama juu ya kiti cha enzi cha mfalme.

7 Mungu ametoa amri:

Milima na vilima visawazishwe, na mabonde yafukiwe, nchi yote iwe tambarare,

Waisraeli watembee salama kwa utukufu wa Mungu.

8 Kwa amri ya Mungu,

vichaka na miti itoayo harufu nzuri itawapa kivuli Waisraeli.

9 Mungu atawaongoza Waisraeli kwa furaha;

kwa mwanga wa utukufu wake, kwa uadilifu utokao kwake mwenyewe.