Upendo wa Mungu wapita hasira yake
1 “Israeli alipokuwa mtoto, nilimpenda,
Kutoka Misri nilimwita mwanangu.
2 Lakini kadiri nilivyozidi kuwaita,
ndivyo walivyozidi kwenda mbali nami;
waliendelea kuyatambikia Mabaali,
na kuvifukizia ubani vinyago vya miungu.
3 Mimi ndiye niliyemfundisha Efraimu kutembea!
Mimi mwenyewe niliwachukua mikononi mwangu;
lakini hawakutambua kuwa mimi ndiye niliyewatunza.
4 Niliwaongoza kwa kamba za huruma
naam, kwa kamba za upendo;
kama baba amwinuaye mtoto mpaka shavuni mwake,
ndivyo nami nilivyokuwa kwao.
Mimi niliinama chini na kuwalisha.
5 Basi, watarudi nchini Misri;
watatawaliwa na mfalme wa Ashuru,
kwa sababu wamekataa kunirudia.
6 “Upanga utavuma katika miji yao,
utavunjavunja miimo ya malango yake
na kuwaangamiza katika ngome zao.
7 Watu wangu wamepania kuniacha mimi,
wakiitwa waje juu,
hakuna hata mmoja anayeweza.
8 Ewe Efraimu, nawezaje kukuacha?
Nawezaje kukutupa ewe Israeli?
Nitawezaje kukufanya kama mji wa Adma?
Nitawezaje kukutenda kama Seboimu!
Nazuiwa na moyo wangu;
huruma yangu imezidi kuwa motomoto.
9 Nitaizuia hasira yangu kali;
sitamwangamiza tena Efraimu,
maana mimi ni Mungu, wala si binadamu.
“Mimi ndimi Mtakatifu miongoni mwenu,
nami sitakuja kuwaangamiza.
10 “Watanifuata mimi Mwenyezi-Mungu ningurumaye kama simba;
nitakaponguruma watanijia toka magharibi wakitetemeka.
11 Watakuja kutoka Misri wakitetemeka kama ndege,
wataruka kutoka Ashuru kama hua
nami nitawarudisha makwao;
mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12 Watu wa Efraimu wananirundikia uongo,
na Waisraeli udanganyifu.
Watu wa Yuda, wananiasi mimi Mungu Mtakatifu.