Hosea 14

Kumrudia Mungu na hali mpya

1 Enyi Waisraeli,

mrudieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

Mmejikwaa kwa sababu ya uovu wenu.

2 Ombeni toba kwake,

mrudieni na kumwambia:

“Utusamehe uovu wote,

upokee zawadi zetu,

nasi tutakusifu kwa moyo.

3 Ashuru haitatuokoa,

hatutategemea tena farasi wa vita.

Hatutaviita tena: ‘Mungu wetu’

hivyo vinyago tulivyochonga wenyewe.

Kwako ee Mungu yatima hupata huruma.”

4 Mwenyezi-Mungu asema,

“Nitaponya utovu wao wa uaminifu;

nitawapenda tena kwa hiari yangu,

maana sitawakasirikia tena.

5 Nitakuwa kama umande kwa Waisraeli

nao watachanua kama yungiyungi,

watakuwa na mizizi kama mwerezi wa Lebanoni.

6 Chipukizi zao zitatanda na kuenea,

uzuri wao utakuwa kama mizeituni,

harufu yao nzuri kama maua ya Lebanoni.

7 Watarudi na kuishi chini ya ulinzi wangu,

watastawi kama bustani nzuri.

Watachanua kama mzabibu,

harufu yao nzuri kama ya divai ya Lebanoni.

8 Enyi watu wa Efraimu,

mna haja gani tena na sanamu?

Mimi ndiye ninayesikiliza sala zenu,

mimi ndiye ninayewatunzeni.

Mimi nitawapa kivuli kama mberoshi,

kutoka kwangu mtapata matunda yenu.

9 Yeyote aliye na hekima ayaelewe mambo haya,

mtu aliye na busara ayatambue.

Maana njia za Mwenyezi-Mungu ni nyofu;

watu wanyofu huzifuata,

lakini wakosefu hujikwaa humo.”