Hosea 6

Toba isiyo ya kweli

1 “ ‘Twendeni, tukamrudie Mwenyezi-Mungu!

Yeye mwenyewe ameturarua,

lakini yeye mwenyewe atatuponya.

Yeye mwenyewe ametujeruhi,

lakini yeye mwenyewe atatibu majeraha yetu.

2 Baada ya siku mbili, atatupa uhai tena,

naam, siku ya tatu atatufufua

ili tuweze kuishi pamoja naye.

3 Basi tumtambue,

tujitahidi kumjua Mwenyezi-Mungu.

Kuja kwake ni hakika kama alfajiri,

yeye atatujia kama manyunyu,

kama mvua za masika ziinyweshayo ardhi.’”

4 Lakini Mwenyezi-Mungu asema hivi:

“Nitakutendea nini ee Efraimu?

Nikufanyie nini ee Yuda?

Upendo wenu kwangu ni kama ukungu wa asubuhi,

kama umande unaotoweka upesi.

5 Ndiyo maana nimewavamia kwa njia ya manabii,

nimewaangamiza kwa maneno yangu,

hukumu yangu huchomoza kama pambazuko.

6 Maana ninachotaka kwenu ni upendo na si tambiko,

Kumjua Mungu na si kutoa sadaka za kuteketezwa.

Uhalifu umeenea kote nchini

7 “Lakini mlilivunja agano langu

kama mlivyofanya mjini Adamu;

huko walinikosea uaminifu.

8 Gileadi ni mji wa waovu,

umetapakaa damu.

9 Kama wanyang’anyi wamwoteavyo mtu njiani,

ndivyo na makuhani walivyojikusanya na kuvizia.

Wanaua watu njiani kuelekea Shekemu,

naam, wanatenda uovu kupindukia.

10 Nimeona jambo la kuchukiza sana

miongoni mwa Waisraeli:

Watu wa Efraimu wanakimbilia miungu mingine

naam, Waisraeli wamejitia unajisi.

11 Nawe Yuda hali kadhalika,

nimekupangia wakati utakapovuna adhabu.