Isaya 15

Mungu ataiangamiza Moabu

1 Kauli ya Mungu dhidi ya nchi ya Moabu.

Mji wa Ari nchini Moabu umeangamizwa usiku;

mji wa Kirinchini Moabu umeteketezwa usiku.

2 Watu wa Diboni wamepanda hekaluni, hadi mahali pa juu kuomboleza,

watu wa Moabu wanalia kwa ajili ya Nebo na Medeba;

vichwa vyote vimenyolewa upara,

ndevu zao zote zimekatwa kabisa.

3 Wanapita njiani wamevaa mavazi ya gunia.

Kwenye paa za nyumba na viwanja vya mji

watu wanalia na kukauka kwa machozi.

4 Watu wa Heshboni na Eleale wanalia,

sauti zao zinasikika hadi Yahazi.

Hata askari wa Moabu wanalia kwa sauti;

mioyo yao inatetemeka.

5 Moyo wangu unasononeka juu ya nchi ya Moabu;

wakimbizi wake wanakimbilia Soari,

wanakimbia mpaka Eglath-shelishiya.

Wanapanda njia ya kwenda Luhithi wakilia,

njiani kwenda Horonaimu wanatoa kilio cha maangamizi.

6 Kijito cha Nimrimu kimekauka;

nyasi zimekauka, majani mabichi yamenyauka,

hakuna chochote kinachoota hapo.

7 Watu wanavuka kijito cha Mierebi

wamebeba mali yao yote waliyochuma,

na kila walichojiwekea kama akiba.

8 Kilio kimezuka pote nchini Moabu,

maombolezo yao yamefika Eglaimu,

naam, yamefika mpaka Beer-elimu.

9 Maji ya Diboni yamejaa damu,

lakini Mungu ataongeza msiba wa Diboni.

Hao wachache watakaobaki hai

na kukimbia kutoka nchini Moabu,

watapelekewa simba wa kuwaua.