Isaya 46

1 “Wewe Beli umeanguka;

Nebo umeporomoka.

Wakati mmoja watu walibeba sanamu zenu.

Sasa wanazibeba mgongoni mwa wanyama,

hao wanyama wachovu wamelemewa.

2 Nyinyi mmeanguka na kuvunjika,

hamwezi kuviokoa vinyago vyenu;

nyinyi wenyewe pia mtapelekwa uhamishoni!

3 “Sikilizeni enyi wazawa wa Yakobo,

nisikilizeni enyi mabaki ya watu wangu wa Israeli.

Mimi niliwatunzeni tangu mlipozaliwa;

niliwabebeni tangu tumboni mwa mama yenu.

4 Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu;

hata katika uzee wenu mimi nitawabeba.

Nilifanya hivyo kwanza,

nitafanya hivyo tena.

Nitawabeba nyinyi na kuwaokoa.

5 “Mtanifananisha na nani, tufanane?

Je, mwaweza kunilinganisha na nani, tulingane?

6 Watu humimina dhahabu kutoka mifuko yao,

hupima fedha kwenye mizani zao,

wakamwajiri mfua dhahabu atengeneze sanamu

kisha huisujudu na kuiabudu!

7 Hujitwisha sanamu hiyo mabegani, wakaibeba,

kisha huiweka mahali pake, ikakaa papo hapo;

kamwe haiwezi hata kusogea kutoka hapo ilipo.

Mtu akiililia, haiwezi kumwitikia,

wala haiwezi kumwokoa mtu katika taabu zake.

8 “Kumbukeni jambo hili na kutafakari,

liwazeni akilini mwenu enyi wakosefu.

9 Kumbukeni mambo niliyotenda hapo kale!

Mimi ndimi Mungu na hakuna mwingine;

naam, mimi ni Mungu, wala hakuna mwingine kama mimi.

10 Nilitangaza mambo ya mwisho tangu mwanzo,

tangu kale nilitangaza mambo yatakayotukia.

Lengo langu litatimia;

mimi nitatekeleza nia yangu yote.

11 Ninamwita tai wangu kutoka mashariki,

naam, msiri wangu kutoka nchi ya mbali.

Mimi nimenena na nitayafanya;

mimi nimepanga nami nitatekeleza.

12 “Nisikilizeni, enyi wenye vichwa vigumu,

nisikilizeni enyi mlio mbali na ukombozi.

13 Siku ya kuwakomboa naileta karibu,

haiko mbali tena;

siku ya kuwaokoeni haitachelewa.

Nitauokoa mji wa Siyoni,

kwa ajili ya Israeli, fahari yangu.