Isaya 52

Mungu ataikomboa Yerusalemu

1 Amka! Amka!

Jipe nguvu zako ewe mji wa Siyoni!

Jivike mavazi yako mazuri,

ewe Yerusalemu, mji mtakatifu.

Maana hawataingia tena kwako

watu wasiotahiriwa na walio najisi.

2 Jikungute mavumbi, uinuke

ewe Yerusalemu uliyetekwa nyara!

Jifungue minyororo yako shingoni,

ewe binti Siyoni uliyechukuliwa mateka.

3 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nyinyi mliuzwa utumwani bila malipo yoyote, na mtakombolewa bila kulipa hata senti moja.

4 Tena mwanzoni nyinyi watu wangu mlikimbilia Misri mkakaa huko. Halafu baadaye Waashuru waliwakandamiza bila sababu yoyote.

5 Katika hali ya sasa napata faida gani kuwaona watu wangu wamepelekwa utumwani? Hao wanaowatawala wanajitapa. Nalo jina langu laendelea kudharauliwa kila siku.

6 Kwa hiyo watu wangu watajua mimi ni nani; siku hiyo watajua kwamba ni mimi ninayesema: Niko!”

7 Tazama inavyopendeza

kumwona mjumbe akitokea mlimani,

ambaye anatangaza amani,

ambaye analeta habari njema,

na kutangaza ukombozi!

Anauambia mji wa Siyoni:

“Mungu wako anatawala!”

8 Sikiliza sauti ya walinzi wako;

wanaimba pamoja kwa furaha,

maana wanaona kwa macho yao wenyewe,

kurudi kwa Mwenyezi-Mungu mjini Siyoni.

9 Pazeni sauti za shangwe, enyi magofu ya Yerusalemu!

Mwenyezi-Mungu amewafariji watu wake,

ameukomboa mji wa Yerusalemu.

10 Mwenyezi-Mungu ameonesha nguvu yake tukufu,

mbele ya mataifa yote.

Atawaokoa watu wake,

na ulimwengu wote utashuhudia.

11 Ondokeni! Ondokeni! Tokeni hapa;

msiguse kitu chochote najisi!

Ondokeni huku Babuloni!

Jitakaseni enyi mbebao vyombo vya Mwenyezi-Mungu.

12 Safari hii hamtatoka kwa haraka,

wala hamtaondoka mbiombio!

Maana Mwenyezi-Mungu atawatangulieni,

Mungu wa Israeli atawalinda kutoka nyuma.

Mtumishi wa Mwenyezi-Mungu

13 Mungu asema hivi:

“Mtumishi wangu atafanikiwa;

atatukuzwa na kupewa cheo,

atapata heshima kuu.

14 Wengi waliomwona walishtuka,

kwa vile sura yake ilikuwa imeharibiwa;

hakuwa tena na umbo la kibinadamu!

15 Lakini sasa ameyashangaza mataifa mengi.

Wafalme wanaduwaa kwa sababu yake,

maana wataona mambo ambayo hawajapata kuambiwa,

na kufahamu mambo ambayo hawajapata kusikia.”