Yeremia 47

Tamko la Mwenyezi-Mungu juu ya Filistia

1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia nabii Yeremia kuhusu Wafilisti, kabla Farao hajaushambulia mji wa Gaza:

2 Mwenyezi-Mungu asema hivi:

“Tazama! Maji yanapanda kutoka kaskazini,

nayo yatakuwa mto uliofurika;

yataifunika nchi nzima na vyote vilivyomo,

mji na wakazi na wanaoishi humo.

Watu watalia,

wakazi wote wa nchi wataomboleza.

3 Watasikia mshindo wa kwato za farasi,

kelele za magari ya vita,

na vishindo vya magurudumu yao.

Kina baba watawasahau watoto wao,

mikono yao itakuwa imelegea mno.

4 Hiyo ni siku ya kuwaangamiza Wafilisti wote,

kukomesha msaada uliobakia kutoka Tiro na Sidoni.

Maana Mwenyezi-Mungu anawaangamiza Wafilisti,

watu waliosalia wa kisiwa cha Kaftori.

5 Watu wa Gaza wamenyoa upara kuomboleza;

mji wa Ashkeloni umeangamia.

Enyi watu wa Anakimu mliobaki

mpaka lini mtajikatakata kwa huzuni?

6 Ee upanga wa Mwenyezi-Mungu!

Utachukua muda gani ndipo utulie?

Ingia katika ala yako,

ukatulie na kunyamaa!

7 Lakini utawezaje kutulia,

hali Mwenyezi-Mungu ameupa kazi?

Ameuamuru ushambulie mji wa Ashkeloni

na watu wanaoishi pwani.”