Sala ya Yona
1 Basi, Yona, akiwa tumboni mwa samaki huyo, akawa akimwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wake,
2 akisema:
“Kwa sababu ya taabu yangu,
nilikuomba, ee Mwenyezi-Mungu,
nawe ukanisikiliza;
toka chini kuzimu, nilikulilia,
nawe ukasikiliza kilio changu.
3 Ulinitupa katika kilindi, katikati ya bahari,
gharika ikanizunguka,
mawimbi na gharika vikapita juu yangu.
4 Nilidhani kwamba nimetengwa nisiwe mbele yako;
nisiweze kuliona tena hekalu lako takatifu.
5 Maji yalinizunguka na kunisonga;
kilindi kilinifikia kila upande,
majani ya baharini yakanifunika kichwa.
6 Niliteremka hadi kwenye misingi ya milima,
katika nchi ambayo milango yake imefungwa milele.
Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu,
umenipandisha hai kutoka humo shimoni.
7 Roho yangu ilipoanza kunitoka,
nilikukumbuka, ee Mwenyezi-Mungu,
sala yangu ikakufikia,
katika hekalu lako takatifu.
8 Watu wanaoabudu sanamu za miungu batili,
huutupilia mbali uaminifu wao kwako.
9 Lakini mimi, kwa wimbo wa shukrani,
nitakutolea sadaka,
na kutimiza nadhiri zangu.
Mwenyezi-Mungu, ndiye aokoaye.”
10 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwamuru yule samaki, naye akamtapika Yona kwenye nchi kavu.