Zaburi 100

Wimbo wa sifa

(Zaburi ya shukrani)

1 Mshangilieni Mwenyezi-Mungu, enyi nchi zote!

2 Mwabuduni Mwenyezi-Mungu kwa furaha,

nendeni kwake mkiimba kwa shangwe!

3 Jueni kwamba Mwenyezi-Mungu ni Mungu.

Yeye ndiye aliyetuumba, nasi ni mali yake;

sisi ni watu wake, ni kondoo wa malisho yake.

4 Pitieni milango ya hekalu lake kwa shukrani,

ingieni katika nyua zake kwa sifa.

Mshukuruni na kulisifu jina lake.

5 Mwenyezi-Mungu ni mwema;

fadhili zake zadumu milele,

na uaminifu wake katika vizazi vyote.