Zaburi 101

Mwongozo mzuri wa mfalme

(Zaburi ya Daudi)

1 Utenzi wangu kuhusu uaminifu na haki;

ninauimba kwa heshima yako, ee Mwenyezi-Mungu.

2 Nitazingatia mwenendo usio na hatia.

Je, utakuja kwangu lini?

Nitaishi kwa unyofu nyumbani kwangu;

3 sitavumilia kamwe upuuzi.

Nayachukia matendo ya watu wapotovu,

mambo yao hayataambatana nami.

4 Upotovu wowote ule uwe mbali nami;

sitahusika kabisa na uovu.

5 Anayemsengenya jirani nitamfutilia mbali;

sitamvumilia mwenye majivuno na kiburi.

6 Nitawaangalia kwa wema watu walio waaminifu,

wapate kuishi pamoja nami.

Watu wanyofu ndio watakaonitumikia.

7 Mwongo yeyote hatakaa nyumbani mwangu;

hakuna msema uongo atakayekaa kwangu.

8 Siku kwa siku nitawaangamiza waovu wote nchini;

nitawaangamiza wabaya wote mjini mwa Mwenyezi-Mungu.