Zaburi 102

Sala katika taabu

(Sala ya mtu aliye katika shida na ambaye anamwekea Mwenyezi-Mungu malalamiko yake)

1 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu,

na kilio changu kikufikie.

2 Usijifiche mbali nami wakati wa taabu!

Unitegee sikio lako,

unijibu upesi wakati ninapokuomba!

3 Siku zangu zapita kama moshi;

mifupa yangu yaungua kama katika tanuri.

4 Nimepondwa moyoni kama nyasi na kunyauka;

sina hata hamu ya chakula.

5 Kutokana na kusononeka kwangu,

nimebaki mifupa na ngozi.

6 Nimekuwa kama ndege wa jangwani;

kama bundi kwenye mahame.

7 Ninalala macho wazi,

kama ndege mkiwa juu ya paa.

8 Mchana kutwa maadui zangu wananisimanga,

wanaonidhihaki hutumia jina langu kulaania.

9 Majivu yamekuwa chakula changu,

machozi nayachanganya na kinywaji changu,

10 kwa sababu ya ghadhabu na hasira yako,

maana umeniokota na kunitupilia mbali.

11 Maisha yangu ni kama kivuli cha jioni;

ninanyauka kama nyasi.

12 Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, watawala milele;

jina lako lakumbukwa vizazi vyote.

13 Wewe utainuka na kuurehemu mji wa Siyoni;

maana wakati umefika wa kuutendea mema;

wakati wake uliopangwa umefika.

14 Watumishi wako wanauthamini sana,

ujapokuwa magofu sasa;

wanauonea huruma,

ingawa umeharibika kabisa.

15 Mataifa yataliheshimu jina la Mwenyezi-Mungu;

wafalme wote duniani wataogopa utukufu wake.

16 Mwenyezi-Mungu ataijenga upya Siyoni,

na kuonekana alivyo mtukufu.

17 Ataikubali sala ya fukara;

wala hatayakataa maombi yao.

18 Andika jambo hili kwa ajili ya vizazi vijavyo;

watakaozaliwa baadaye wamsifu Mwenyezi-Mungu.

19 Kwamba aliangalia chini kutoka patakatifu pake juu,

Mwenyezi-Mungu aliangalia dunia kutoka mbinguni,

20 akasikia lalamiko la wafungwa;

akawaachilia huru waliohukumiwa kuuawa.

21 Hivyo watu watatangaza jina la Mwenyezi-Mungu huko Siyoni;

sifa zake zitatangazwa huko Yerusalemu,

22 wakati mataifa yatakapokusanyika pamoja

na falme zitakutana kumwabudu Mwenyezi-Mungu.

23 Mungu amenipunguzia nguvu ningali kijana;

ameyafupisha maisha yangu.

24 Ee Mungu wangu, usinichukue sasa

wakati ningali bado kijana.

Ee Mwenyezi-Mungu wewe wadumu milele.

25 Wewe uliiumba dunia zamani za kale,

mbingu ni kazi ya mikono yako.

26 Hizo zitatoweka, lakini wewe wabaki;

hizo zitachakaa kama vazi.

Utazitupilia mbali kama nguo,

nazo zitapotelea mbali.

27 Lakini wewe ni yuleyule daima,

na maisha yako hayana mwisho.

28 Watoto wa watumishi wako watakaa salama;

wazawa wao wataimarishwa mbele yako.