Kumtumainia Mungu
(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)
1 Kwake Mwenyezi-Mungu nakimbilia usalama;
mnawezaje basi kuniambia:
“Ruka kama ndege, mpaka milimani,
2 maana waovu wanavuta pinde;
wameweka mishale tayari juu ya uta,
wawapige mshale watu wema gizani!
3 Kama misingi ikiharibiwa,
mtu mwadilifu atafanya nini?”
4 Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu;
kiti cha enzi cha Mwenyezi-Mungu kiko mbinguni.
Kwa macho yake huwachungulia wanadamu,
na kujua kila kitu wanachofanya.
5 Mwenyezi-Mungu huwapima waadilifu na waovu;
huwachukia kabisa watu wakatili.
6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto na madini ya kiberiti;
upepo wa hari utakuwa ndio adhabu yao.
7 Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu na apenda uadilifu;
watu wanyofu watakaa pamoja naye.