Zaburi 110

Kutawazwa kwa mfalme mteule

(Zaburi ya Daudi)

1 Mwenyezi-Mungu amwambia bwana wangu:

“Keti upande wangu wa kulia,

hata niwaweke maadui zako chini ya miguu yako.”

2 Mwenyezi-Mungu ataeneza enzi yako kutoka Siyoni;

utatawala juu ya maadui zako wote.

3 Watu wako watakujia kwa hiari,

siku utakapokwenda kuwapiga maadui.

Juu ya milima mitakatifu watakujia vijana wako,

kama umande unaotokeza alfajiri mapema.

4 Mwenyezi-Mungu amekuapia wala hatabadili nia yake:

“Wewe ni kuhani milele kwa utaratibu wa ukuhani wa Melkisedeki.”

5 Bwana yuko upande wako wa kulia;

atawaponda wafalme atakapokasirika.

6 Atayahukumu mataifa na kuwaua watu wengi;

atawaponda viongozi kila mahali duniani.

7 Mfalme atakunywa maji ya kijito njiani;

naye atainua kichwa juu kwa ushindi.