Zaburi 111

Mungu asifika kwa matendo yake

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!

Nitamshukuru Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote,

nikijumuika na jamii ya watu waadilifu.

2 Matendo ya Mwenyezi-Mungu ni makuu mno!

Wote wanaoyafurahia huyatafakari.

3 Kila afanyacho kimejaa utukufu na fahari;

uadilifu wake wadumu milele.

4 Amesababisha matendo yake ya ajabu yakumbukwe;

Mwenyezi-Mungu ni mwema na mwenye huruma.

5 Huwapa chakula wenye kumcha;

hasahau kamwe agano lake.

6 Amewaonesha watu wake nguvu ya matendo yake,

amewapa nchi za mataifa mengine ziwe mali yao.

7 Matendo yake ni ya haki na ya kuaminika;

kanuni zake zote ni za kutegemewa.

8 Amri zake zadumu daima na milele;

zimetolewa kwa haki na uadilifu.

9 Aliwakomboa watu wake

na kufanya nao agano la milele.

Yeye ni mtakatifu na wa kutisha mno!

10 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa hekima;

wote wanaozitii amri zake hujaliwa busara.

Sifa zake zadumu milele.