Zaburi 113

Sifa kwa Mungu mtukufu

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!

Enyi watumishi wa Mwenyezi-Mungu, lisifuni jina lake!

2 Jina lake litukuzwe,

sasa na hata milele.

3 Kutoka mashariki na hata magharibi,

litukuzwe jina la Mwenyezi-Mungu!

4 Mwenyezi-Mungu atawala juu ya mataifa yote,

utukufu wake wafika juu ya mbingu.

5 Nani aliye kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu?

Yeye ameketi juu kabisa;

6 lakini anatazama chini,

azione mbingu na dunia.

7 Humwinua fukara kutoka mavumbini;

humnyanyua maskini kutoka unyonge wake,

8 na kumweka pamoja na wakuu;

pamoja na wakuu wa watu wake.

9 Humjalia mwanamke tasa furaha nyumbani kwake;

humfurahisha kwa kumjalia watoto.

Msifuni Mwenyezi-Mungu!