Mungu mmoja wa kweli
1 Sio sisi, ee Mwenyezi-Mungu, sio sisi;
bali wewe peke yako utukuzwe,
kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako.
2 Kwa nini mataifa yaseme:
“Mungu wenu yuko wapi?”
3 Mungu wetu yuko mbinguni;
yeye hufanya yote anayotaka.
4 Miungu yao ni ya fedha na dhahabu;
imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu.
5 Ina vinywa, lakini haisemi.
Ina macho, lakini haioni.
6 Ina masikio, lakini haisikii.
Ina pua, lakini hainusi.
7 Ina mikono, lakini haipapasi.
Ina miguu, lakini haitembei.
Haiwezi kamwe kutoa sauti.
8 Wote wanaoitengeneza wanafanana nayo,
kadhalika na wote wanaoitumainia.
9 Enyi Waisraeli, mtumainieni Mwenyezi-Mungu;
yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.
10 Enyi wazawa wa Aroni, mtumainieni Mwenyezi-Mungu;
yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.
11 Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, mtumainini,
yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.
12 Mwenyezi-Mungu atukumbuka na atatubariki;
atawabariki watu wa Israeli,
atawabariki wazawa wa Aroni.
13 Atawabariki wote wamchao,
atawabariki wakubwa na wadogo.
14 Mwenyezi-Mungu awajalieni muongezeke;
awajalieni muongezeke nyinyi na wazawa wenu!
15 Mbarikiwe na Mwenyezi-Mungu,
aliyeziumba mbingu na dunia.
16 Mbingu ni mali yake Mwenyezi-Mungu,
bali dunia amewapa binadamu.
17 Wafu hawamsifu Mwenyezi-Mungu,
wala wale wanaoshuka katika nchi ya kimya.
18 Lakini sisi tulio hai twamsifu Mwenyezi-Mungu;
tutamsifu sasa na hata milele.
Msifuni Mwenyezi-Mungu!