Zaburi 12

Kuomba msaada

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Sheminithi. Zaburi ya Daudi)

1 Fanya haraka, ee Mwenyezi-Mungu!

Watu wema wamekwisha;

waaminifu wametoweka miongoni mwa watu.

2 Kila mmoja humdanganya mwenzake,

husema kwa kudanganya na kwa moyo wa unafiki.

3 Ee Mwenyezi-Mungu

uikomeshe hiyo midomo ya udanganyifu,

na ndimi hizo zinazojigamba kupindukia.

4 Wao husema: “Kwa ndimi zetu tutashinda;

midomo tunayo, nani awezaye kututawala?”

5 Lakini Mwenyezi-Mungu asema:

“Kwa sababu maskini wanadhulumiwa,

na wahitaji wanapiga kite, sasa naja,

nami nitawapa usalama wanaoutazamia.”

6 Neno la Mwenyezi-Mungu ni safi,

safi kama fedha iliyosafishwa katika tanuri,

naam, kama fedha iliyosafishwa mara saba.

7 Utulinde, ee Mwenyezi-Mungu,

utukinge daima na kizazi hiki kiovu.

8 Waovu wanazunguka kila mahali;

upotovu unatukuzwa kati ya watu.