Zaburi 121

Mungu kinga yetu

(Wimbo wa Kwenda Juu, wa Daudi)

1 Natazama juu milimani;

msaada wangu utatoka wapi?

2 Msaada wangu watoka kwa Mwenyezi-Mungu,

aliyeumba mbingu na dunia.

3 Hatakuacha uanguke;

mlinzi wako hasinzii.

4 Kweli mlinzi wa Israeli

hasinzii wala halali.

5 Mwenyezi-Mungu ni mlinzi wako;

yuko upande wako wa kulia kukukinga.

6 Mchana jua halitakuumiza,

wala mwezi wakati wa usiku.

7 Mwenyezi-Mungu atakukinga na baya lolote;

atayalinda salama maisha yako.

8 Mwenyezi-Mungu atakulinda katika shughuli zako zote

tangu sasa na hata milele.