Zaburi 122

Sifa za Yerusalemu

(Wimbo wa Kwenda Juu, wa Daudi)

1 Nilifurahi waliponiambia:

“Twende nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu.”

2 Sasa tuko tumesimama,

kwenye malango yako, ee Yerusalemu!

3 Yerusalemu, mji uliojengwa,

ili jumuiya ikutane humo.

4 Humo ndimo makabila yanamofika,

naam, makabila ya Israeli,

kumshukuru Mwenyezi-Mungu kama alivyoagiza.

5 Humo mmewekwa mahakama ya hukumu ya haki,

mahakama ya ukoo wa kifalme wa Daudi.

6 Uombeeni Yerusalemu amani:

“Wote wakupendao na wafanikiwe!

7 Ndani ya kuta zako kuwe na amani,

majumbani mwako kuweko usalama!”

8 Kwa ajili ya jamaa na ndugu zangu,

ee Yerusalemu, nakutakia amani!

9 Kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu,

ninakuombea upate fanaka!