Zaburi 124

Mungu kinga yetu

(Wimbo wa Kwenda Juu, wa Daudi)

1 “Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu

Semeni nyote mlio katika Israeli:

2 “Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu,

wakati ule tuliposhambuliwa na maadui,

3 hakika tungalimezwa tukiwa hai,

wakati hasira zao zilipotuwakia.

4 Tungalikumbwa na gharika,

tungalifunikwa na mto wa maji,

5 mkondo wa maji ungalituchukua!”

6 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu,

ambaye hakutuacha makuchani mwao.

7 Tumeponyoka kama ndege mtegoni;

mtego umeteguliwa, nasi tukaokoka.

8 Msaada wetu watoka kwa Mwenyezi-Mungu,

aliyeumba mbingu na dunia.