Zaburi 127

Bila Mungu kazi ya binadamu haifai

(Wimbo wa Kwenda Juu, wa Solomoni)

1 Mwenyezi-Mungu asipoijenga nyumba,

waijengao wanajisumbua bure.

Mwenyezi-Mungu asipoulinda mji,

waulindao wanakesha bure.

2 Mnajisumbua bure kuamka mapema asubuhi

na kuchelewa kwenda kupumzika jioni,

mjipatie chakula kwa jasho lenu.

Mungu huwaruzuku walio wake hata walalapo.

3 Watoto ni riziki kutoka kwa Mwenyezi-Mungu;

watoto ni tuzo lake kwetu sisi.

4 Watoto waliozaliwa wazazi wakiwa bado vijana,

ni kama mishale mikononi mwa askari.

5 Heri mtu aliye na mishale hiyo kwa wingi.

Hatashindwa atakapokabiliana na adui mahakamani.