Zaburi 13

Kuomba msaada

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)

1 Mpaka lini ee Mwenyezi-Mungu, utanisahau?

Je, utanisahau mpaka milele?

Mpaka lini utanificha uso wako?

2 Nitakuwa na wasiwasi rohoni hadi lini,

na sikitiko moyoni siku hata siku?

Hadi lini adui zangu watafurahia taabu zangu?

3 Uniangalie na kunijibu, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu.

Uyaangazie macho yangu, nisipatwe na usingizi wa kifo.

4 Usiwaache maadui zangu waseme: “Tumemweza huyu!”

Watesi wangu wasije wakafurahia kuanguka kwangu.

5 Lakini mimi nazitumainia fadhili zako;

moyo wangu na ufurahie wokovu wako.

6 Nitakuimbia wewe, ee Mwenyezi-Mungu,

kwa ukarimu mwingi ulionitendea!