Zaburi 135

Sifa kwa Mungu

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!

Lisifuni jina la Mwenyezi-Mungu,

msifuni enyi watumishi wake.

2 Msifuni enyi mkaao katika nyumba yake,

ukumbini mwa nyumba ya Mungu wetu!

3 Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema;

mtukuzeni kwa nyimbo maana inafaa.

4 Mwenyezi-Mungu amemchagua Yakobo kuwa wake,

nyinyi watu wa Israeli kuwa mali yake mwenyewe.

5 Najua hakika kuwa Mwenyezi-Mungu ni mkuu;

Bwana wetu ni mkuu juu ya miungu yote.

6 Mwenyezi-Mungu hufanya chochote anachotaka,

mbinguni, duniani, baharini na vilindini.

7 Ndiye aletaye mawingu kutoka mipaka ya dunia;

afanyaye gharika kuu kwa umeme,

na kuvumisha upepo kutoka ghala zake.

8 Ndiye aliyewaua wazaliwa wa kwanza huko Misri,

wazaliwa wa watu na wanyama kadhalika.

9 Ndiye aliyefanya ishara na maajabu kwako, ee Misri,

dhidi ya Farao na maofisa wake wote.

10 Ndiye aliyeyaangamiza mataifa mengi,

akawaua wafalme wenye nguvu:

11 Kina Sihoni mfalme wa Waamori,

Ogu mfalme wa Bashani,

na wafalme wote wa Kanaani.

12 Alichukua nchi zao na kuwapa watu wake;

naam, ziwe riziki ya watu wake Israeli.

13 Jina lako, ee Mwenyezi-Mungu, ladumu milele,

utakumbukwa kwa fahari nyakati zote.

14 Mwenyezi-Mungu atawatetea watu wake;

na kuwaonea huruma watumishi wake.

15 Miungu ya uongo ya mataifa ni fedha na dhahabu,

imetengenezwa kwa mikono ya binadamu.

16 Ina vinywa, lakini haisemi;

ina macho, lakini haioni.

17 Ina masikio, lakini haisikii;

wala haiwezi hata kuvuta pumzi.

18 Wote walioifanya wafanane nayo,

naam, kila mmoja anayeitegemea!

19 Enyi watu wa Israeli, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu!

Enyi makuhani, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu!

20 Enyi Walawi, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu!

Enyi wachaji wa Mwenyezi-Mungu, mtukuzeni!

21 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu katika Siyoni,

atukuzwe katika makao yake Yerusalemu.

Msifuni Mwenyezi-Mungu!