Sala ya kuomba ulinzi wa Mungu
(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)
1 Ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe na watu wabaya,
unikinge na watu wakatili.
2 Watu hao huwaza mabaya daima,
huzusha magomvi kila mara.
3 Ndimi zao hatari kama za nyoka;
midomoni mwao mna maneno ya sumu kama ya joka.
4 Ee Mwenyezi-Mungu, unilinde na makucha ya wabaya;
unikinge na watu wakatili
ambao wamepanga kuniangusha.
5 Wenye kiburi wamenitegea mitego,
wametandaza kamba kama wavu,
wameficha mitego njiani wanikamate.
6 Namwambia Mwenyezi-Mungu, “Wewe ndiwe Mungu wangu.”
Usikilize, ee Mwenyezi-Mungu, sauti ya ombi langu.
7 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wangu, mkombozi wangu mkuu,
umenikinga salama wakati wa vita.
8 Ee Mwenyezi-Mungu, usiwape waovu wanayotaka;
wala mipango yao mibaya usiifanikishe.
9 Hao wanaonizingira wanainua vichwa;
uovu wa maneno yao uwapate wao wenyewe!
10 Makaa ya moto yawaangukie;
watumbukizwe mashimoni, wasiinuke tena.
11 Wanaowasengenya wengine wasifanikiwe katika nchi;
uovu uwapate wakatili na kuwaangamiza mara!
12 Najua Mwenyezi-Mungu hutetea kisa cha wanaoteswa,
na kuwapatia haki maskini.
13 Hakika waadilifu watalisifu jina lako;
wanyofu watakaa kwako.