Zaburi 141

Hatari za tamaa mbaya

(Zaburi ya Daudi)

1 Nakuita, ee Mwenyezi-Mungu,

uje haraka kunisaidia!

Uisikilize sauti yangu wakati ninapokuita!

2 Sala yangu uipokee kama ubani;

niinuapo mikono yangu kwako unikubali kama tambiko ya jioni.

3 Ee Mwenyezi-Mungu ukilinde kinywa changu,

uweke ulinzi mlangoni mwa mdomo wangu.

4 Unikinge nisielekee kufanya mabaya,

nisijishughulishe na matendo maovu;

nisijiunge na watu watendao mabaya,

wala nisishiriki kamwe karamu zao.

5 Afadhali mtu mwema anipige kunionya;

lakini sikubali kamwe kusifiwa na wabaya,

maana nasali daima dhidi ya maovu yao.

6 Wakuu wao watakapopondwa miambani,

ndipo watatambua maneno yangu yalikuwa sawa.

7 Mifupa yao itatawanywa mdomoni pa Kuzimu

kama kuni zilizopasuliwa vipandevipande!

8 Bali mimi nakutegemea, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu;

ninakimbilia usalama kwako, usiniache hatarini.

9 Unikinge na mitego waliyonitegea,

uniepushe na matanzi ya hao watu waovu.

10 Waovu wanaswe katika mitego yao wenyewe,

wakati mimi najiendea zangu salama.