Zaburi 146

Sifa kwa Mungu Mwokozi

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!

Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee nafsi yangu!

2 Nitamsifu Mwenyezi-Mungu maisha yangu yote;

nitamwimbia Mungu wangu muda wote niishipo.

3 Msiwategemee wakuu wa dunia;

hao ni binadamu tu, hawawezi kuokoa.

4 Binadamu akitoa pumzi yake ya mwisho,

anarudi mavumbini alimotoka;

na hapo mipango yake yote hutoweka.

5 Heri mtu anayesaidiwa na Mungu wa Yakobo,

mtu aliyeweka tumaini lake kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wake,

6 aliyeumba mbingu na dunia,

bahari na vyote vilivyomo.

Yeye hushika ahadi yake milele.

7 Yeye huwapatia wanaoonewa haki zao,

huwapa wenye njaa chakula.

Mwenyezi-Mungu huwapa wafungwa uhuru,

8 huwafungua macho vipofu.

Mwenyezi-Mungu huwainua waliokandamizwa;

huwapenda watu walio waadilifu.

9 Mwenyezi-Mungu huwalinda wageni,

huwategemeza wajane na yatima;

lakini huipotosha njia ya waovu.

10 Mwenyezi-Mungu atawala milele,

Mungu wako, ee Siyoni, ni mfalme vizazi vyote!

Msifuni Mwenyezi-Mungu!