Zaburi 15

Rafiki ya Mungu

(Zaburi ya Daudi)

1 Nani ee Mwenyezi-Mungu atakayekaa hemani mwako?

Nani atakayeishi juu ya mlima wako mtakatifu?

2 Ni mtu aishiye bila lawama,

atendaye daima yaliyo mema,

asemaye ukweli kutoka moyoni;

3 ni mtu asiyesengenya watu,

asiyemtendea uovu rafiki yake,

wala kumfitini jirani yake;

4 ni mtu anayewadharau wafisadi,

lakini huwaheshimu wamchao Mwenyezi-Mungu;

ni mtu asiyegeuza kiapo chake hata kikimtia hasara;

5 asiyekopesha fedha yake kwa riba,

wala kupokea rushwa kumdhulumu asiye na hatia.

Mtu atendaye hayo,

kamwe hatatikisika.