Zaburi 2

Mfalme mteule wa Mungu

1 Kwa nini mataifa yanafanya ghasia?

Mbona watu wanafanya njama za bure?

2 Wafalme wa dunia wanajitayarisha;

watawala wanashauriana pamoja,

dhidi ya Mwenyezi-Mungu na mteule wake.

3 Wanasema: “Tujiondoe katika utawala wao;

tutupilie mbali minyororo yao!”

4 Mwenyezi-Mungu atawalaye juu mbinguni,

anawacheka na kuwadhihaki.

5 Kisha, anawakaripia kwa ghadhabu,

na kuwatisha kwa hasira, akisema:

6 “Nimemtawaza mfalme niliyemteua,

anatawala Siyoni, mlima wangu mtakatifu!”

7 Mfalme asema: “Nitatangaza azimio la Mwenyezi-Mungu.

Mungu aliniambia:

‘Wewe ni mwanangu,

mimi leo nimekuwa baba yako.

8 Niombe nami nitakupa mataifa yawe urithi wako,

na dunia nzima kuwa mali yako.

9 Utawaponda kwa fimbo ya chuma;

utawavunja kama chungu cha mfinyanzi!’”

10 Sasa enyi wafalme, tumieni busara;

sikilizeni onyo hili, enyi watawala wa dunia.

11 Mtumikieni Mwenyezi-Mungu kwa uchaji;

12 msujudieni na kutetemeka;

asije akakasirika, mkaangamia ghafla;

kwani hasira yake huwaka haraka.

Heri yao wote wanaokimbilia usalama kwake!