Zaburi 23

Mungu mchungaji wangu

(Zaburi ya Daudi)

1 Mwenyezi-Mungu ni mchungaji wangu,

sitapungukiwa na kitu.

2 Hunipumzisha kwenye malisho mabichi;

huniongoza kando ya maji matulivu,

3 na kuirudishia nafsi yangu nguvu mpya.

Huniongoza katika njia sawa

kwa hisani yake.

4 Nijapopita katika bonde la giza kuu la kifo,

sitaogopa hatari yoyote,

maana wewe ee Mwenyezi-Mungu u pamoja nami;

gongo lako na fimbo yako vyanilinda.

5 Umeniandalia karamu mbele ya maadui zangu;

umenipaka mafuta kichwani pangu;

kikombe changu umekijaza mpaka kufurika.

6 Kweli wema wako na fadhili zako zitakuwa pamoja nami,

siku zote za maisha yangu;

nami nitakaa nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu milele.