Zaburi 25

Kumwomba Mungu uongozi na ulinzi

(Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, kwako naielekeza nafsi yangu!

2 Nakutumainia wewe, ee Mungu wangu,

usiniache niaibike;

adui zangu wasifurahie kushindwa kwangu.

3 Usimwache anayekutumainia apate aibu;

lakini waaibike wote wanaokuasi kwa makusudi.

4 Unijulishe njia zako, ee Mwenyezi-Mungu;

unifundishe nifuate unayotaka.

5 Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha,

kwani wewe ni Mungu, mwokozi wangu;

ninakutegemea wewe kila siku.

6 Uikumbuke huruma yako ee Mwenyezi-Mungu;

uzikumbuke na fadhili zako kuu,

ambazo zimekuwako tangu kale.

7 Usikumbuke dhambi na makosa ya ujana wangu;

unikumbuke kadiri ya fadhili zako,

kwa ajili ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu.

8 Mwenyezi-Mungu ni mwema na mnyofu,

kwa hiyo huwafundisha wenye dhambi njia.

9 Huwaongoza wanyenyekevu katika uadilifu;

naam, huwafundisha hao njia yake.

10 Mwenyezi-Mungu hutenda kwa fadhili na uaminifu,

kwa wale wanaoshika agano lake na maamuzi yake.

11 Kwa ajili ya jina lako, ee Mwenyezi-Mungu,

unisamehe kosa langu kwani ni kubwa.

12 Kila mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu,

Mwenyezi-Mungu atamfunza njia ya kufuata.

13 Mtu wa namna hiyo atafanikiwa daima,

na wazawa wake watamiliki nchi.

14 Mwenyezi-Mungu ni rafiki ya wale wamchao;

yeye huwajulisha hao agano lake.

15 Namwangalia Mwenyezi-Mungu daima;

yeye atainasua miguu yangu mtegoni.

16 Unielekee, ee Mungu, unionee huruma,

maana mimi ni mpweke na mnyonge.

17 Uniondolee mahangaiko ya moyoni mwangu;

unitoe katika mashaka yangu.

18 Uangalie mateso yangu na dhiki yangu;

unisamehe dhambi zangu zote.

19 Angalia jinsi walivyo wengi maadui zangu;

ona jinsi wanavyonichukia kwa ukatili.

20 Uyalinde maisha yangu, uniokoe;

nakimbilia usalama kwako,

usikubali niaibike.

21 Wema na uadilifu vinihifadhi,

maana ninakutumainia wewe.

22 Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli;

uwaokoe katika taabu zao zote.