Zaburi 28

Kuomba msaada

(Zaburi ya Daudi)

1 Nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu!

Ewe mwamba wa usalama wangu usiniwie kama kiziwi,

la sivyo kama usiponisikiliza,

nitakuwa kama wale washukao shimoni kwa wafu.

2 Sikiliza sauti ya ombi langu,

ninapokulilia unisaidie,

ninapoinua mikono yangu kuelekea maskani yako takatifu.

3 Usinipatilize pamoja na watu wabaya,

pamoja na watu watendao maovu:

Watu wasemao na wenzao maneno ya amani,

kumbe wamejaa uhasama moyoni.

4 Uwaadhibu kadiri ya matendo yao,

kufuatana na maovu waliyotenda.

Waadhibu kadiri ya matendo yao wenyewe;

uwatendee yale wanayostahili.

5 Hawajali matendo ya Mwenyezi-Mungu;

hawatambui mambo aliyoyafanya.

Kwa sababu hiyo atawabomoa,

wala hatawajenga tena upya.

6 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu,

maana amesikiliza ombi langu.

7 Mwenyezi-Mungu ndiye nguvu yangu na ngao yangu;

tegemeo la moyo wangu limo kwake.

Amenisaidia nami nikashangilia kwa moyo;

kwa wimbo wangu ninamshukuru.

8 Mwenyezi-Mungu ni nguvu ya watu wake;

yeye ni kimbilio la wokovu kwa mfalme wake mteule.

9 Ee Mungu, uwaokoe watu wako;

uwabariki watu hao walio mali yako.

Uwe mchungaji wao na kuwategemeza milele.