Zaburi 30

Sala ya shukrani

(Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, nakutukuza maana umeniokoa,

wala hukuwaacha maadui zangu wanisimange.

2 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu,

nilikulilia msaada, nawe ukaniponya.

3 Ee Mwenyezi-Mungu, umeniokoa kutoka kuzimu;

umenipa tena uhai,

umenitoa miongoni mwa waendao kuzimu.

4 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa, enyi waaminifu wake;

kumbukeni utakatifu wake na kumshukuru.

5 Hasira yake hudumu kitambo kidogo,

wema wake hudumu milele.

Kilio chaweza kuwapo hata usiku,

lakini asubuhi huja furaha.

6 Mimi nilipofanikiwa, nilisema:

“Kamwe sitashindwa!”

7 Kwa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu,

umeniimarisha kama mlima mkubwa.

Lakini ukajificha mbali nami,

nami nikafadhaika.

8 Nilikulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu;

naam niliomba dua kwako ee Mwenyezi-Mungu:

9 “Je, utapata faida gani nikifa

na kushuka hadi kwa wafu?

Je, mavumbi ya wafu yanaweza kukusifu?

Je, yanaweza kusimulia uaminifu wako?

10 Usikie, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie;

ee Mwenyezi-Mungu, unisaidie!”

11 Wewe umegeuza maombolezo langu kuwa ngoma ya furaha;

umeniondolea huzuni yangu, ukanizungushia furaha.

12 Mimi nitakusifu wala sitakaa kimya.

Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu nitakushukuru milele.