Zaburi 38

Sala katika mateso

(Zaburi ya Daudi ya matoleo)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako;

usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2 Mishale yako imenichoma;

mkono wako umenigandamiza.

3 Hamna mahali nafuu mwilini mwangu,

kwa sababu umenikasirikia;

hamna penye afya hata mifupani mwangu,

kwa sababu ya dhambi yangu.

4 Nimefunikwa kabisa na dhambi zangu,

zinanilemea kama mzigo mzito mno kwangu.

5 Madonda yangu yameoza na kunuka,

na hayo ni matokeo ya ujinga wangu.

6 Nimepindika mpaka chini na kupondeka;

mchana kutwa nazunguka nikiomboleza.

7 Viungo vyangu vimeshambuliwa na homa;

mwilini mwangu hamna nafuu yoyote.

8 Nimelegea na kupondekapondeka;

nasononeka kwa kusongwa moyoni.

9 Ee Bwana, wewe wajua tazamio langu lote;

kwako hakikufichika kilio changu.

10 Moyo wanidunda, nguvu zimeniishia;

hata macho yangu nayo yamekwisha fifia.

11 Rafiki na wenzangu wanaepa kuona mateso yangu,

na jamaa zangu wanakaa mbali nami.

12 Wanaotaka kuniua wanatega mitego yao;

wanaonitakia niumie wanatishia kuniangamiza.

Mchana kutwa wanafanya mipango dhidi yangu.

13 Lakini mimi nimekuwa kama kiziwi, sisikii;

nimekuwa kama bubu asiyeweza kusema kitu.

14 Naam, nimekuwa kama mtu asiyesikia,

kama mtu asiye na chochote cha kujitetea.

15 Lakini ninakutumainia wewe, ee Mwenyezi-Mungu;

wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, ndiwe utakayenijibu.

16 Nakuomba tu maadui wasinisimange,

wasione fahari juu ya kuanguka kwangu.

17 Karibu sana nitaanguka;

nakabiliwa na maumivu ya daima.

18 Naungama uovu wangu;

dhambi zangu zanisikitisha.

19 Maadui zangu hawajambo, wana nguvu;

ni wengi mno hao wanaonichukia bure.

20 Hao wanaonilipa maovu kwa wema wangu,

wananipinga kwa sababu natenda mema.

21 Usinitupe, ee Mwenyezi-Mungu;

ee Mungu wangu, usikae mbali nami.

22 Uje haraka kunisaidia;

ewe Mwenyezi-Mungu, uliye wokovu wangu.