Zaburi 42

Sala ya Mkimbizi

(Kwa Mwimbishaji. Utenzi wa Wakorahi)

1 Kama paa atamanivyo maji ya kijito,

ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu!

2 Naona kiu ya Mungu, kiu ya Mungu aliye hai.

Nitafika lini kwake na kuuona uso wake?

3 Machozi yamekuwa chakula changu mchana na usiku,

waliponiambia kila siku: “Yuko wapi Mungu Wako!”

4 Nakumbuka tena mambo haya

kwa majonzi moyoni mwangu:

Jinsi nilivyokwenda na umati wa watu,

nikawaongoza kwenda nyumbani kwa Mungu

wakipiga vigelegele vya shukrani;

umati wa watu wakifanya sherehe!

5 Mbona nasononeka hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu?

Nitamtumainia Mungu,

maana nitamsifu tena

yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.

6 Nimesongwa na huzuni moyoni mwangu,

kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu,

kutoka katika eneo la Yordani,

kutoka mlima Hermoni na Mizari.

7 Nimeporomoshewa mafuriko ya maji

mafuriko ya maji yaja karibu

nayo yaita maporomoko mapya.

Mawimbi na mapigo yako yamenikumba.

8 Mwenyezi-Mungu atanijalia fadhili zake mchana;

nami nimwimbie wimbo wa sifa usiku,

nimwombe Mungu anipaye uhai.

9 Namwambia Mungu, mwamba wangu:

“Kwa nini umenisahau?

Yanini niende huko na huko nikiomboleza

kwa kudhulumiwa na adui yangu?”

10 Nimepondwa kwa matukano yao,

wanaponiuliza kila siku:

“Yuko wapi, Mungu wako!”

11 Mbona nasononeka hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo?

Nitamtumainia Mungu,

maana nitamsifu tena Mungu,

aliye msaada wangu na Mungu wangu.