Zaburi 46

Mungu yuko upande wetu

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi. Mtindo wa Alamothi)

1 Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu;

yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.

2 Kwa hiyo hatutaogopa chochote,

dunia ijapoyeyuka

na milima kutikisika kutoka baharini;

3 hata kama bahari ikichafuka na kutisha,

na milima ikatetemeka kwa machafuko yake.

4 Kuna mto ambao maji yake hufurahisha mji wa Mungu,

makao matakatifu ya Mungu Mkuu.

5 Mungu yumo mjini humo, nao hauwezi kutikiswa;

Mungu ataupa msaada alfajiri na mapema.

6 Mataifa yaghadhibika na tawala zatikisika;

Mungu anguruma nayo dunia yayeyuka.

7 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi,

Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

8 Njoni mwone matendo ya Mwenyezi-Mungu;

oneni maajabu aliyoyafanya duniani.

9 Hukomesha vita popote duniani,

huvunjavunja pinde na mikuki,

nazo ngao huziteketeza.

10 Asema: “Nyamazeni na kujua kuwa mimi ni Mungu!

Mimi natukuka katika mataifa yote;

mimi natukuzwa ulimwenguni kote!”

11 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi,

Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.