Zaburi 47

Mungu, Mfalme wa ulimwengu wote

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi)

1 Enyi watu wote, pigeni makofi!

Msifuni Mungu kwa sauti za shangwe!

2 Maana Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu, anatisha.

Yeye ni Mfalme mkuu wa ulimwengu wote.

3 Ametuwezesha kuwashinda watu wa mataifa,

ameyaweka mataifa chini ya mamlaka yetu.

4 Ametuchagulia nchi hii iwe urithi wetu,

ambayo ni fahari ya Yakobo anayempenda.

5 Mungu amepanda juu na vigelegele,

Mwenyezi-Mungu na sauti ya tarumbeta.

6 Mwimbieni Mungu sifa, mwimbieni!

Mwimbieni mfalme wetu sifa, mwimbieni!

7 Mwimbieni Mungu sifa kwa tenzi;

maana yeye ni mfalme wa ulimwengu wote.

8 Mungu anayatawala mataifa yote;

amekaa katika kiti chake cha enzi kitakatifu.

9 Viongozi wa watu wa mataifa wanakusanyika,

wanajiunga na watu wa Mungu wa Abrahamu,

maana nguvu zote duniani ni zake Mungu,

yeye ametukuka sana.