Zaburi 53

Mtu asiyemcha Mungu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Mahalathi. Utenzi wa Daudi)

1 Wapumbavu hujisemea moyoni:

“Hakuna Mungu!”

Wote wamepotoka kabisa,

wametenda mambo ya kuchukiza;

hakuna hata mmoja atendaye jema.

2 Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni,

aone kama kuna yeyote mwenye busara,

kama kuna yeyote anayemtafuta Mungu.

3 Lakini wote wamekosa,

wote wamepotoka pamoja,

hakuna atendaye mema,

hakuna hata mmoja.

4 “Je, hao watendao maovu hawana akili?

Wanawatafuna watu wangu kama mikate;

wala hawanijali mimi Mungu!”

5 Hapo watashikwa na hofu kubwa,

hofu ambayo hawajapata kuiona;

maana Mungu ataitawanya mifupa ya adui,

hao wataaibika maana Mungu amewakataa.

6 Laiti ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Siyoni!

Mungu atakaporekebisha hali ya watu wake,

wazawa wa Yakobo watashangilia;

Waisraeli watafurahi.