Zaburi 54

Sala ya kujikinga na maadui

(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Utenzi wa Daudi wakati mtu mmoja kutoka Zifu alipomwendea Shauli na kumjulisha kuwa Daudi amejificha kwao.)

1 Uniokoe, ee Mungu, kwa jina lako;

unitetee kwa nguvu yako.

2 Uisikie, ee Mungu, sala yangu;

uyategee sikio maneno ya kinywa changu.

3 Watu wenye kiburi wananishambulia;

wakatili wanayawinda maisha yangu,

watu ambao hawamjali Mungu.

4 Najua Mungu ni msaada wangu,

Mwenyezi-Mungu hutegemeza maisha yangu.

5 Yeye atawaadhibu maadui zangu kwa uovu wao wenyewe;

kwa uaminifu wako, ee Mungu, uwaangamize.

6 Nitakutolea tambiko kwa moyo mkunjufu;

nitakushukuru kwa kuwa ni vema.

7 Maana umeniokoa katika taabu zangu zote,

nami nimewaona maadui zangu wameshindwa.