Zaburi 56

Kumtumainia Mungu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Njiwa Mkimya wa Mbali”. Utenzi wa Daudi baada ya kukamatwa na Wafilisti kule Gathi)

1 Ee Mungu, unionee huruma,

maana watu wananishambulia.

Mchana kutwa maadui wananidhulumu.

2 Mchana kutwa maadui zangu wananishambulia;

ni wengi mno hao wanaonipiga vita.

3 Ee Mungu Mkuu, hofu inaponishika,

mimi nakutumainia wewe.

4 Namtumainia Mungu na kusifu neno lake;

namtumainia Mungu, wala siogopi.

Binadamu dhaifu atanifanya nini?

5 Mchana kutwa wanapotosha kisa changu;

mawazo yao yote ni ya kunidhuru.

6 Wanakutana kupanga na kunivizia;

wanachunguza yote nifanyayo;

wananiotea kwa shabaha ya kuniua.

7 Ee Mungu, uwalipe kwa kadiri ya uovu wao,

uwaangushe hao waovu kwa hasira yako.

8 Wewe wakujua kusukwasukwa kwangu;

waweka kumbukumbu ya machozi yangu yote.

Je, yote si yamo kitabuni mwako?

9 Kila mara ninapokuomba msaada wako,

maadui zangu wanarudishwa nyuma.

Najua kweli Mungu yuko upande wangu.

10 Namtumaini Mungu na kusifu neno lake;

namtumainia Mwenyezi-Mungu na kusifu neno lake.

11 Namtumainia Mungu, wala siogopi.

Binadamu atanifanya nini?

12 Ee Mungu, nitatimiza ahadi zangu kwako;

nitakutolea tambiko za shukrani,

13 Maana umeniokoa katika kifo,

naam, umenilinda nisianguke chini;

nipate kuishi mbele yako, ee Mungu,

katika mwanga wa uhai.