Zaburi 57

Kuomba msaada

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Usiharibu!” Utenzi wa Daudi alipomponyoka Shauli na kujificha pangoni)

1 Unihurumie, ee Mungu, unihurumie,

maana kwako nakimbilia usalama.

Kivulini mwa mabawa yako nitakimbilia usalama,

hata hapo dhoruba ya maangamizi itakapopita.

2 Namlilia Mungu Mkuu,

Mungu anikamilishiaye nia yake.

3 Atanipelekea msaada toka mbinguni na kuniokoa;

atawaaibisha hao wanaonishambulia.

Mungu atanionesha fadhili zake na uaminifu wake!

4 Mimi nimezungukwa na maadui,

wenye uchu wa damu kama simba;

meno yao ni kama mikuki na mishale,

ndimi zao ni kama panga kali.

5 Utukuzwe, ee Mungu, juu ya mbingu!

Utukufu wako uenee duniani kote!

6 Maadui wamenitegea wavu waninase,

nami nasononeka kwa huzuni.

Wamenichimbia shimo njiani mwangu,

lakini wao wenyewe wametumbukia humo.

7 Niko thabiti moyoni, ee Mungu,

naam, niko thabiti moyoni;

nitaimba na kukushangilia!

8 Amka, ee nafsi yangu!

Amkeni, enyi kinubi na zeze!

Nitayaamsha mapambazuko!

9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa;

nitakuimbia sifa kati ya mataifa.

10 Fadhili zako zaenea hata juu ya mbingu,

uaminifu wako wafika hata mawinguni.

11 Utukuzwe, ee Mungu, juu ya mbingu!

Utukufu wako uenee duniani kote!