Zaburi 58

Mungu hakimu wa mahakimu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Usiharibu”. Utenzi wa Daudi)

1 Enyi watawala,je, mwahukumu kwa haki kweli?

Je, mnawahukumu watu kwa adili?

2 La! Nyinyi mwafikiria tu kutenda maovu;

nyinyi wenyewe mwaeneza dhuluma nchini.

3 Waovu wamepotoka tangu kuzaliwa kwao,

waongo hao, wamekosa tangu walipozaliwa.

4 Wana sumu kama sumu ya nyoka;

viziwi kama joka lizibalo masikio,

5 ambalo halisikii hata sauti ya mlozi,

au utenzi wa mganga stadi wa uchawi.

6 Ee Mungu, wavunje meno yao,

yangoe, ee Mwenyezi-Mungu, meno ya simba hao.

7 Watoweke kama maji yanayodidimia mchangani,

kama nyasi wakanyagwe na kunyauka,

8 watoweke kama konokono ayeyukavyo,

kama mimba iliyoharibika isiyoona kamwe jua!

9 Kabla hawajatambua, wangolewe

kama miiba, michongoma au magugu.

Kwa hasira ya Mungu, wapeperushwe mbali,

wakiwa bado hai.

10 Waadilifu watafurahi waonapo waovu wanaadhibiwa;

watatembea katika damu ya watu wabaya.

11 Watu wote watasema: “Naam, waadilifu hupata tuzo!

Hakika yuko Mungu anayeihukumu dunia!”