Zaburi 61

Kuomba ulinzi

(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mungu, usikie kilio changu,

usikilize sala yangu.

2 Ninakulilia kutoka miisho ya dunia,

nikiwa nimevunjika moyo.

Uniongoze juu kwenye mwamba mkubwa

3 maana wewe ndiwe kimbilio langu,

kinga yangu imara dhidi ya adui.

4 Naomba nikae nyumbani mwako milele

nipate usalama chini ya mabawa yako.

5 Ee Mungu, umezisikia ahadi zangu,

umenijalia sehemu yangu unayowapa wale wakuchao.

6 Umjalie mfalme maisha marefu,

miaka yake iwe ya vizazi vingi.

7 Atawale milele mbele yako, ee Mungu;

fadhili na uaminifu wako vimlinde.

8 Hivyo nitakuimbia nyimbo za sifa,

nikizitekeleza ahadi zangu kila siku.