Zaburi 62

Mungu mlinzi wangu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi)

1 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu,

kwake watoka wokovu wangu.

2 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu,

yeye ni ngome yangu, sitatikisika.

3 Hata lini mtanishambulia mimi?

Hata lini nyinyi nyote mtanipiga,

mimi niliye kama kiambaza kilichoinama,

kama ukuta unaoanza kubomoka?

4 Mmepanga kuniangusha toka mahali pangu pa heshima;

furaha yenu ni kusema uongo.

Kwa maneno, mnabariki,

lakini moyoni mnalaani.

5 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu;

kwake naliweka tumaini langu.

6 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu,

yeye ni ngome yangu, sitatikisika.

7 Wokovu na fahari yangu vyatoka kwa Mungu;

mwamba wangu mkuu na kimbilio langu ni Mungu.

8 Enyi watu, mtumainieni Mungu daima;

mfungulieni Bwana yaliyo moyoni mwenu.

Mungu ndiye kimbilio la usalama wetu.

9 Binadamu wote ni kama pumzi tu;

wote, wakubwa kwa wadogo, hawafai kitu.

Tena ukiwapima uzito hawafikii kilo,

wote pamoja ni wepesi kuliko pumzi.

10 Msitegemee dhuluma,

msijisifie mali ya wizi;

kama mali zikiongezeka, msizitegemee.

11 Mungu ametamka mara moja,

nami nimesikia tena na tena:

Kwamba enzi ni mali yake Mungu;

12 naam, nazo fadhili ni zake Bwana;

humlipa kila mtu kadiri ya matendo yake.