Zaburi 63

Hamu ya kuwa pamoja na Mungu

(Zaburi ya Daudi wakati alipokuwa katika jangwa la Yudea)

1 Ee Mungu, wewe u Mungu wangu,

nami nakutafuta kwa moyo;

roho yangu inakutamani kama mtu mwenye kiu;

nina kiu kama nchi kavu isiyo na maji.

2 Nimetaka kukuona patakatifuni pako,

niione nguvu yako na utukufu wako.

3 Fadhili zako ni bora kuliko maisha,

nami nitakusifu kwa mdomo wangu.

4 Nitakushukuru maisha yangu yote;

nitainua mikono yangu na kukuomba.

5 Roho yangu inafurahi kama kwa karamu na vinono;

kwa shangwe nitaimba sifa zako.

6 Niwapo kitandani ninakukumbuka,

usiku kucha ninakufikiria;

7 maana wewe umenisaidia daima.

Kivulini mwa mabawa yako nitashangilia.

8 Roho yangu inaambatana nawe kabisa,

mkono wako wa kulia wanitegemeza.

9 Lakini hao wanaotaka kuyaangamiza maisha yangu,

watatumbukia chini kwenye makao ya wafu.

10 Watauawa kwa upanga,

watakuwa chakula cha mbweha.

11 Lakini mfalme atafurahi kwa sababu ya Mungu;

wanaoahidi kwa jina la Mungu watamsifu,

lakini vinywa vya waongo vitafumbwa.