Zaburi 64

Sala ya kuomba ulinzi wa Mungu

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)

1 Usikie, ee Mungu, lalamiko langu;

yalinde maisha yangu na vitisho vya maadui.

2 Unikinge na njama za waovu,

na ghasia za watu wabaya.

3 Wananoa ndimi zao kama upanga,

wanafyatua maneno ya ukatili kama mishale.

4 Toka mafichoni wamshambulia mtu mnyofu,

wanamshambulia ghafla bila kuogopa.

5 Wanashirikiana katika nia yao mbaya;

wanapatana mahali pa kuficha mitego yao.

Wanafikiri: “Hakuna atakayeweza kuiona.”

6 Hufanya njama zao na kusema:

“Sasa tumekamilisha mpango!

Nani atagundua hila zetu?”

Mipango ya siri imefichika moyoni mwa mtu!

7 Lakini Mungu atawapiga mishale,

na kuwajeruhi ghafla.

8 Atawaangamiza kwa sababu ya maneno yao;

kila atakayewaona atatikisa kichwa.

9 Hapo watu wote wataogopa;

watatangaza aliyotenda Mungu,

na kufikiri juu ya matendo yake.

10 Waadilifu watafurahi kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu,

na kukimbilia usalama kwake;

watu wote wanyofu wataona fahari.