Zaburi 70

Kuomba msaada

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi ya matoleo ya ukumbusho)

1 Upende kuniokoa ee Mungu!

Ee Mwenyezi-Mungu, uje haraka kunisaidia.

2 Wanaonuia kuniangamiza,

na waaibike na kufedheheka!

Hao wanaotamani niumie,

na warudi nyuma na kuaibika.

3 Hao wanaonisimanga,

na wapumbazike kwa kushindwa kwao.

4 Lakini wote wale wanaokutafuta,

wafurahi na kushangilia kwa sababu yako.

Wapendao wokovu wako,

waseme daima: “Mungu ni mkuu!”

5 Nami niliye maskini na fukara,

unijie haraka, ee Mungu!

Ndiwe msaada wangu na mkombozi wangu;

ee Mwenyezi-Mungu, usikawie!