Zaburi 75

Mungu hakimu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Usiharibu”. Zaburi ya Asafu. Wimbo)

1 Tunakushukuru, ee Mungu,

tunakushukuru!

Tunatangaza ukuu wa jina lako

na kusimulia juu ya matendo yako makuu.

2 Mungu asema: “Mimi nimeweka wakati maalumu!

Wakati huo nitahukumu kwa haki.

3 Nchi ikitetemeka na vyote vilivyomo,

mimi ndiye ninayeitegemeza misingi yake.

4 Nawaambia wenye kiburi:

‘Acheni kujigamba’;

na waovu: ‘Msioteshe pembe za kiburi!

5 Msijione kuwa watu wa maana sana,

wala kusema maneno ya majivuno.’”

6 Hukumu haitoki mashariki au magharibi;

wala haitoki nyikani au mlimani.

7 Mungu mwenyewe ndiye hakimu;

humshusha mmoja na kumkweza mwingine.

8 Mwenyezi-Mungu, anashika kikombe mkononi,

kimejaa divai kali ya hasira yake;

anaimimina na waovu wote wanainywa;

naam, wanainywa mpaka tone la mwisho.

9 Lakini mimi nitafurahi milele,

nitamwimbia sifa Mungu wa Yakobo.

10 Atavunja nguvu zote za watu waovu;

lakini nguvu za waadilifu ataziimarisha.