Zaburi 84

Hamu ya kuwa nyumbani kwa Mungu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Gitithi. Zaburi ya Wakorahi)

1 Jinsi gani yanavyopendeza makao yako,

ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi!

2 Nafsi yangu yatamani mno maskani ya Mwenyezi-Mungu!

Moyo na mwili wangu wote wamshangilia Mungu aliye hai.

3 Hata shomoro wamepata makao yao,

mbayuwayu wamejenga viota vyao,

humo wameweka makinda yao,

katika madhabahu zako, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi,

Mfalme wangu na Mungu wangu!

4 Heri wale wanaokaa nyumbani mwako,

wakiimba daima sifa zako.

5 Heri watu wanaopata nguvu zao kwako,

wanaotamani kwenda kuhiji mlimani kwako.

6 Wapitapo katika bonde kavu la Baka,

hulifanya kuwa mahali pa chemchemi,

na mvua za vuli hulijaza madimbwi.

7 Wanaendelea kupata nguvu zaidi na zaidi;

watamwona Mungu wa miungu huko Siyoni.

8 Usikie sala yangu ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi;

unitegee sikio, ee Mungu wa Yakobo.

9 Ee Mungu, umwangalie kwa wema ngao yetu mfalme,

umtazame huyo uliyemweka wakfu kwa mafuta.

10 Siku moja tu katika maskani yako,

ni bora kuliko siku elfu mahali pengine;

afadhali kusimama mlangoni pa nyumba yako,

kuliko kuishi nyumbani kwa watu waovu.

11 Mwenyezi-Mungu ni jua letu na ngao yetu;

yeye hutuneemesha na kutujalia fahari.

Hawanyimi chochote kilicho chema,

wale waishio kwa unyofu.

12 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi,

heri mtu yule anayekutumainia wewe!