Zaburi 87

Sifa ya Yerusalemu

(Zaburi ya Wakorahi. Wimbo)

1 Mungu amejenga mji wake

juu ya mlima wake mtakatifu.

2 Mwenyezi-Mungu anaupenda mji wa Siyoni,

kuliko makao mengine ya Yakobo.

3 Mambo ya fahari yanasemwa juu yako, ee mji wa Mungu:

4 “Miongoni mwa wale wanijuao mimi,

wapo watu wa Misrina Babuloni.

Kadhalika Filistia, Tiro na Kushi,

wote walizaliwa kwako!”

5 Na kuhusu Siyoni itasemwa:

“Siyoni ni mama wa huyu na huyu;

Mungu Mkuu atauthibitisha.”

6 Mwenyezi-Mungu ataandika katika kitabu,

atakapoorodhesha watu:

“Huyu amezaliwa huko!”

7 Wote wanacheza ngoma na kuimba:

“Siyoni, chanzo chetu ni kwako.”